,./.,

,,

... ...

';';';';

''=

==

adv
Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

Friday, May 8, 2015




Muswada wa sheria ya makosa ya kimtandao ya Tanzania (Cyber Crimes Act 2015) ni ‘draconian law’ ambayo kiuhalisia imechelewa sana kuja hasa kutokana na maendeleo hasi na chanya ambayo ni makubwa kwa nchi yetu ya “dunia ya tatu”. Ni jambo la hatari mno kwa taifa changa na masikini kuwa na ongezeko kubwa la matumizi ya teknolojia ya mawasiliano bila kuwa na sheria ambayo itasimamia usalama wa watumiaji na ustawi wa nchi kwa ujumla. Muswada huu unaainisha makosa yanayohusiana na matumizi ya mfumo wa kompyuta na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, kuweka utaratibu wa upelelezi, ukusanyaji na matumizi ya ushahidi wa kieletroniki.


Watu wengi wamejitokeza kuupinga mswada huu ambao umeshasainiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania. Sheria hii itakuwa ikitumika kuanzia bara na visiwani huku ikijaribu kusimamia makosa ambayo yanaweza kutokana na matumizi mabaya ya mitandao.

Watu wengi wamejitokeza kuipinga hasa wale “wanaharakati” wenye imani ya haki ya mtu kuzungumza au kupata habari bila vikwazo.  Hali kadhalika tulishuhudia watetezi wa haki za binadamu pamoja na wawakilishi wa watumiaji wa Mtandao wa intaneti nchini wakitoa sababu zenye “uzito” za kwanini sheria hii ipite kwa hati ya dharura na bila ya kupata majibu. Wakaendelea kuwa Muswada huu ambao kati ya “makosa” mengi uliyonayo kubwa moja wapo ni majukumu makubwa aliyopewa Mkuu wa Kituo chochote cha Polisi kuwa na uwezo wa kupekuwa na kuchukua vielelezo/data pale anaposhuku kuna suala la uhalifu unaohusu mtandao.

Kiukweli nimeshangazwa sana na hawa wanaharakati wa hii nchi,woga wa hii sheria unatokana na nini? Hii nchi inatakiwa isimamiwe,ilindwe na istawishwe kwa gharama yoyote hata kwa kuathiri baadhi ya maslahi ya vikundi mbalimbali vya kijamii. Inabidi tukubaliane kwamba nchi kwanza,amani ya nchi na ustawi wake unatakiwa kulindwa kwa asilimia mia moja bila kujali maslahi ya “wanaharakati” wa kiafrika ambao wapo kwa ajili ya kusimamia maslahi ya wafadhili wao ambao ni mataifa kutoka nje.

Kuna ubaya gani wa kukamatwa kwa mtu anaye sambaza taarifa za uongo,uchochezi na udhalilishaji? Ni nani asiyejua madhara ya taarifa za uzushi kwa jamii? Kwa nini tusikubaliane kuwa tunahitajika kuwa wakweli katika utoaji taarifa zetu kwa manufaa ya nchi yetu? Nini umuhimu wa matumizi ya teknolojia ya mawasiliano kwa mtanzania wakati zaidi ya asilimia themanini ya mawasiliano yetu ni yale yasiyo zalishi (Non-Productive)? Nchi iliyojaa blogu za picha za ngono na mapenzi,habari za uzushi na zenye kashfa,matusi na zisizo na maadili kwa nini sheria hii sio muhimu? Watu wanatumia majina yasiyo yao (fake) kwa ajili ya kutukana wenzao,makundi mbalimbali katika mitandao kwa ajili ya kutumiana picha za uchi na udhalilishaji,kweli hii sheria haina umuhimu kwa hili? Nchi hii ina blogu ngapi zinazohusu maswala ya Uchumi  kama Kilimo,Uvuvi,mazingira, Ufugaji na kadhalika? Kwa nini huu usiwe mwanzo wa kuhamasisha uanzishwaji wa blogu na makundi mbalimbali ya mtandaoni yenye dhima chanya ya kimaendeleo? Kwa nini watu hawazungumziii kuhusu umuhimu au uzuri wa hii sheria?

Nchi hii imegeuka ya watu kulalamika kila siku,watu wanalalamika kuhusu mkuu wa kituo kuwa na haki ya kuchunguza kifaa chako kama komputa hasa pale anapokutilia shaka bila hati ya mahakama,ubaya wa hii sheria ni nini kama wewe ni msafi na hauna makosa? Ni vipi kama kifungu hiki  kinasaidia kukamata magaidi wanaojiandaa kulipua eneo fulani hapa Tanzania hasa baada ya kutiliwa shaka? Itakuwa yenye msaada au la? Kwa nini tupo katika mawazo hasi muda wote? Kwani tukienda nchi za watu huko hawatukagui? Mbona hatulalamiki? Ni watumiaji wangapi wa mitandao wanatumia hii kama ni fursa katika maendeleo? Sheria inahusu wale wenye nia ya kufanya makosa,kwa nini uwe muoga? Kama unaipenda nchi hii na huna maslahi binafsi basi huna sababu ya kuipinga sana sheria hii maana hakuna anaye kataa kuwa haina mapungufu lakini inaweza kuwa mwanzo mzuri wa kuelekea kwenye maendeleo mazuri ya matumizi ya mitandao.

Watu wanatakiwa watambue kuwa matumizi mabaya ya mitandao yanaweza kusababisha maafa makubwa kama tulivyoona katika nchi mbalimbali za Afrika kama Rwanda, Burundi,Afrika ya Kusini na nchi nyingine nyingi ambapo,usambazaji wa taarifa za uongo na au chochezi ulisababisha mvurugano na upotevu wa amani kwa takribani zaidi ya miongo miwili sasa wanahangaika kukaa vikao kurudisha hiyo amani. Tukubaliane kuwa “Freedom of Speech” ni muhimu sana kwa nchi ila amani,ulinzi na ustawi wa nchi ni muhimu zaidi kuliko hiyo “freedom of speech” ya baadhi ya makundi ya watu.

Pia najua kuwa mataifa makubwa duniani hususani ya Ulaya na huyo Marekani, hawatafurahishwa kabisa na sheria hii kwani wao Uhuru wa habari ni muhimu kuliko ustawi au usalama wa nchi. Kwao ni bora nchi ya kiafrika iwe na machafuko,njaa, magonjwa au umaskini wa kutupwa kuliko kukosa “freedom of Speech” hata kama inahatarisha uhai wa Taifa. Tumejionea mengi,wakijitahidi kuwafadhili “wanaharakati wetu” katika kupigania mambo mbalimbali ambayo wao wananufaika au ina maslahi kwa namna moja au nyingine.

Tupiganie nchi yetu ipate taarifa sahihi na salama kwa ajili ya ustawi wa nchi na sio bora habari ambazo zinaweza kuleta machafuko katika nchi yetu. Tungependa kuwa na vikundi, magazeti, tovuti na blogu zinazotupa taarifa sahihi na zenye kujenga kama kilimo bora, uvuvi salama na jinsi ya kuondoa umaskini katika jamii yetu na sio taarifa za picha za uchi,maiti,chochezi,uongo wenye nia ya kugombanisha watu na kuondoa kabisa hali ya utulivu. Watu wajifunze kuwa na nidhamu ya kuishi,nchi kama Korea,Indonesia,Malaysia, China na nyinginezo zimeweza kudhibiti makosa mbalimbali ya kimtandao ambayo sasa yameshika hatamu na kufanikiwa kutumia mitandao kwa faida ya watu na jamii kwa ujumla.

Ndugu mtanzania jiulize,kwa siku unapokea ujumbe mara ngapi? Ni asilimia ngapi ya ujumbe ni wa maana ambao unakuwa sahihi na wenye kujenga? Ni vikundi vingapi vya kwenye mitandao tulivyonavyo vinakuwa vikizungumzia mambo mbalimbali mazuri wa mustakabali wa Taifa letu? Sheria imekuja kuleta nidhamu ya sisi katika kutumia mitandao kwani ukiacha unafiki utakubaliana nami kuwa tumekosa nidhamu katika matumizi ya mitandao na tunahitaji mahala pa kuanzia,japo sio pakamilifu lakini yatupasa kukubaliana kuwa sharti tuanze kama msemavyo “better late than never”.   

Hivyo basi,hebu tuache kudanganyana na tuisome sheria kwa uzuri, nimechoka na wizi wa mitandao na benki zetu,pia Sheria hii haina tofauti na sheria za nchi nyingine,sisi hatuko kisiwani,tunaishi na wahalifu hivyo tunahitaji sheria kali kwa ajili ya kujilinda kwa manufaa yetu kisiasa,uchumi na jamii. Usifuate mkumbo na kuishia kutafuta vifungu vichache kwa ajili ya kukosoa kwa maslahi yako binafsi na kuacha vingine vyenye nia ya kujenga.
Mwandishi Thabithy Bashiri anapatikana kwa thabeethy@gmail.com +255 717 451213

0 comments:

Post a Comment

ufunguzi